ELIMU: MSHINDI WA TAJI LA MISS TZ 2012, BRIGITTE ALFRED, JAT KUWASOMESHA ALBINO 50 NCHINI
https://jaridahuru.blogspot.com/2014/08/elimu-mshindi-wa-taji-la-miss-tz-2012.html
WALEMAVUwa ngozi (Albino) 50 wanatarajiwa kupewa mafunzo ya ujasiriamali kuanzia Agosti 18, jijini Dar es Salaam.
Mafunzo hayo yanaratibiwa na Taasisi ya Brigitte Alfred Foundation (BAF) inayomilikiwa na aliyekuwa Miss Tanzania 2012, Brigitte Alfred kwa kushirikiana na Taasisi ya Junior Achievement Tanzania (JAT).
Akizungumza katika uzinduzi wa programu hiyo uliofanyika jana, Brigitte alisema mafunzo hayo yanalenga namna ya kujitambua, kutathmini aina mbalimbali za biashara, kutunza pesa, kuandika mchanganuo wa biashara, kutembelea sehemu mbalimbali zinazoendana na biashara na jinsi ya kuanza biashara.
“Mafunzo haya yatachukua muda wa mwaka mmoja, kila mshiriki wa mafunzo haya atapatiwa kitabu chenye masomo yote ili aweze kuendelea kujisomea,” alisema Brigitte.
Mkurugenzi wa JAT, Maria Ngowi alisema kuwa wamejipanga kufanikisha mpango huo na wanaamini watakaopata mafunzo hayo watafanikiwa katika maisha yao.
Alisema JAT imejikita katika nyanja tatu ambazo ni ujasiriamali, elimu ya kuzalisha, kuwekeza na kutunza fedha na elimu ya kazi.
Ngowi alisema JAT ni sehemu ya taasisi kubwa ulimwenguni ya Junior Achievement International, ambayo iko katika nchi 120 duniani huku Afrika ikiwa katika nchi 17.