KITAIFA: SAKATA LA MCHECHU SHIRIKA LA NYUMBA (NHC) LAGEUKA MTEGO WA PANYA, UKWELI, VIGOGO WAWEKWA WAZI
https://jaridahuru.blogspot.com/2014/07/kitaifa-sakata-la-mchechu-shirika-la.html
Mchechu katika moja ya kongamano |
SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC), limesema bado Mkurugenzi wake, Nehemia Mchechu na menejimenti yake wana mikataba halali ambayo haijamalizika muda wake kama inavyodaiwa na mitandao mbalimbali ya kijamii.
Kauli hiyo imekuja siku chache tangu kusambaa kwa habari katika gazeti moja (si Tanzania Daima), na mitandao mbalimbali ya kijamii kwamba, mkurugenzi huyo kwa sasa analiongoza shirika hilo kinyume na sheria baada ya muda wake kuisha.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kaimu Mkurugenzi wa NHC, David Shambwe, alisema habari hizo zinazodaiwa kutoka ndani ya bodi ya shirika hilo ni za kupika, zilizolenga kudhoofisha utendaji kazi wa mkurugenzi huyo ambaye amebadili sura nzima ya shirika hilo tangu alipokabidhiwa nafasi hiyo.
Shambwe alisema jamii inapaswa kuelewa kwamba bodi inayolishwa maneno hayo ni kwamba tangu iingie madarakani miezi miwili iliyopita, haijawahi kukaa katika kikao chochote kujadili suala la kumuondoa mkurugenzi wala kupunguza menejimenti ya shirika iliyopo sasa.
Kuhusu kutokuwepo kwa Mchechu kwenye ufunguzi wa miradi, alidai kwamba hakukutokana na kuwepo kwa mizengwe kama ilivyoripotiwa, bali wanachofahamu alikuwa katika likizo yake ya mwaka iliyoanza Juni 30 na kumalizika Julai 18, mwaka huu.
“Likizo hii ni stahili halali ya Mchechu kama walivyo watumishi wengine wa umma, ambapo baada ya kumalizika alianza kazi kwa kuwa safarini kuanzia Julai 21 na anatarajiwa kuwepo ofisini rasmi Julai 28, mwaka huu,” alifafanua Shambwe.
Pia, alitumia fursa hiyo kuwaondoa wasiwasi wateja wao kuwa hakuna mtafaruku wowote ndani ya shirika hilo, na kuahidi kwamba wataendelea kuwapa huduma zao zilizo bora katika sekta ya nyumba waliyoaminiwa na taifa kuisimamia.
Tanzania Daima ilifanya jitihada za kumtafuta Mwenyekiti wa Bodi ya NHC, Zakia Meghji kwa njia ya simu ili kujua ukweli kuhusu sakata hilo, lakini simu yake iliita bila ya kupokewa hata pale alipotumiwa ujumbe mfupi hakujibu.