jaridahuru

Mitandao

SIASA: UCHU WA KITI CHA RAIS 2015 WAITAPANYA SERIKALI, YAGAWANYIKA KATIKA MAKUNDI KUFUATA WAGOMBEA

http://freemedia.co.tz/daima/wp-content/uploads/2014/07/urais.jpg

 
 
MHEMUKO wa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakiwemo viongozi wa serikali kukimbilia kutangaza nia ya kumrithi Rais Jakaya Kikwete mwakani, umezigawa taasisi mbalimbali za serikali, binafsi na umma hivyo kuzorotesha utendaji wa kila siku.

Hivi karibuni, baadhi ya wanachama wa CCM wamekuwa wakitamka hadharani nia zao za kuwania urais mwakani, huku wakijinasibu kwa hoja mbalimbali.

Baadhi ya wana CCM waliotangaza nia ya kuwania urais mwakani ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Fredrick Sumaye, Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba huku Edward Lowassa, Bernad Membe, William Ngeleja, Steven Wassira wakitajwa matendo yao kuonyesha nia hiyo.

Wakati ikiwa hivyo huku chama tawala kikishindwa kudhibiti, hali hiyo imeanza kuzorotesha utendaji serikalini kwa kile kinachoelezwa watendaji kugawanyika kulingana na wagombea hao.
Uchunguzi wa Tanzania Daima unaonyesha kuwa baadhi ya watendaji serikalini wanashindwa kutekeleza majukumu  yao  ipasavyo au wanalazimika kutekeleza baadhi ya mambo kwa hofu ya kuonekana wako upande wa mtangaza nia fulani.

“Ndugu yangu, hivi sasa kwa kweli tuko mtegoni, maana ukifanya hiki hata kama kina nia nzuri unajihisi kama kitampendeza nani kati ya wanaoonyesha kugombea urais mwakani, na mbaya zaidi, baadhi yao wamekuwa wakitutamkia wazi kuwa tunachokifanya tuko upande wa fulani wakati kumbe sie hatuko huko… hii inatutia hofu na tunatekeleza majukumu yetu kwa hofu badala ya kuzingatia taaluma, taratibu, kanuni na sheria,” alisema mtendaji mmoja katika Wilaya ya Korogwe ambaye aliomba jina lihifadhiwe kwa maslahi ya kibarua chake.

Chanzo kingine kiliipasha Tanzania Daima kuwa hali hiyo ya hofu si tu kwa watendaji wa serikali, bali pia hata kwa taasisi nyingine, ikiwamo vyama na mashirikisho ya michezo ambayo pia yanaathiriwa na harakati za urais mwakani.

Kilisema kuwa pia mpango wa diplomasia ya michezo ulioibuliwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa kwa mara ya kwanza mwaka huu tangu nchi kupata uhuru, una mlengo wa kisiasa zaidi hususan kuelekea uchaguzi mkuu wa mwakani.

“Suala la programu za maandalizi na hata ushiriki wa timu za taifa nje ya nchi kimsingi ziko kwenye wizara yenye dhamana na michezo, sasa kitendo hiki cha Wizara ya Mambo ya Nje kinaonekana kuishusha wizara husika ya michezo, kwani mipango hiyo ilitakiwa kufanywa na wizara yenye dhamana na michezo, hivyo badala ya kuonekana ni jambo la kujenga limeibua chuki miongoni mwa watendaji wa wizara hizo,” kilisema chanzo chetu.

Inaelezwa tayari vyama na mashirikisho mbalimbali ya michezo yameingia katika mkumbo huo na kujikuta yakitumika na baadhi ya waonyesha nia ya kugombea urais mwakani, jambo linalowagawa viongozi na hivyo kuzorotesha ufanisi.

Chanzo hicho, kilitaja baadhi ya mashirikisho ya michezo ambayo yameingia kwenye mtego wa wagombea urais mwakani ni pamoja na Shirikisho la Soka  Tanzania (TFF), Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), klabu kongwe ya Simba, klabu ya wasanii wa maigizo (Bongo Movie), kampuni na taasisi mbalimbali zinazojishughulisha na masuala mbalimbali ya kijamii.

Inaelezwa kuwa kitendo cha Rais wa TFF, Jamal Malinzi na Rais wa Simba, Evans Aveva kumtembelea Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, kimekuwa nongwa, kwamba kinawaathiri wao binafsi na taasisi wanazoongoza kwa madai kuwa wanamuunga mkono kuelekea uchaguzi mkuu mwakani.

Watu kutoka ndani ya mashirikisho na klabu ya Simba, wanaeleza kuwa kuna baadhi ya mipango ilikuwa ifanikishwe kupitia mashirika mbalimbali ya umma na binafsi imesitishwa, kisa kikiwa hatua ya viongozi hao kuonekana na mmoja wa wanaotajwa kuwania urais mwakani.

“Kwa kweli kuelekea uchaguzi wa mwakani ni lawama, maana tunashindwa kutekeleza majukumu yetu itakiwavyo, ukifanya hivi unaambiwa uko kambi ya fulani, ukitaka kumwalika mgeni rasmi katika matukio yetu, suala la urais mwakani linawekwa kipaumbele, kwa kweli siasa inatutia hofu, inatuchanganya na inatugawa,” alisema mmoja wa viongozi wa michezo.

Inaelezwa kitendo cha Rais wa RT, Anthony Mtaka, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya (DC) ya Mvomero mkoani Morogoro kuishambulia waziwazi Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kwamba ni dhaifu siku ya kuagwa kwa wanamichezo wa Tanzania kwenda kwenye kambi ya mazoezi nje ya nchi kujiandaa na michezo ya Jumuiya ya Madola, Glasgow, Scotland kilikuwa na mlengo wa kuelekea uchaguzi mkuu wa mwakani.

Timu za ngumi, riadha, judo, kunyanyua vitu vizito na mpira wa meza ziliagwa Aprili 29, mwaka huu kwenye ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere, ambako mgeni rasmi alikuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Membe.

Akitoa neno la shukrani, Rais wa RT, Mtaka, mbali na kummwagia sifa Waziri Membe, wasaidizi wake na wizara yake kwa ujumla kwa kufanikisha kambi hizo za nje ya nchi kupitia mpango huo wa diplomasia ya michezo, katika hali ya kushangaza na kushtua aliiponda waziwazi wizara yenye dhamana na michezo na kudai imegeuka wizara ya kulipana mishahara tu, hivyo ibadilike na iige wizara ya Waziri Membe.

Kauli hiyo ilionekana kuwashtua na kuwaweka kwenye butwaa Waziri Membe, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo, Leonard Thadeo ambaye alimwakilisha waziri mwenye dhamana na michezo, Naibu Mkurugenzi wa Michezo, Juliana Yasoda ambaye pia alikuwa ni mshehereshaji siku hiyo na baadhi ya wanamichezo na wadau waliohudhuria hafla hiyo.

Katika kuweka sawa, kwa unyonge Yasoda alieleza kuwa wote ni serikali kwa maana ya wizara hizo, na kwamba ziara hiyo ya mafunzo nje ya nchi imefanikishwa na wizara hizo.

Kauli hiyo ya Mtaka, inaelezwa ililenga kumbeba Membe na kuidhalilisha Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, jambo ambalo hadi sasa limejenga chuki hususan katika suala  hilo  la michezo ya Madola.

“Haiwezekani, kuna kitu, Mtaka licha ya kuwa kiongozi wa michezo, ni kiongozi wa serikali, kimsingi haikuwa busara kukiponda na kukidhalilisha mbele ya jamii chombo kingine cha serikali, kule ni kuvuana nguo na kuna ajenda,” alisema ofisa mmoja wa wizara yenye dhamana na michezo.
Harakati za wanachama wa CCM kuutaka urais mapema kabla hata taratibu ndani ya chama kuwekwa hadharani, zimekuwa zikipigiwa kelele na baadhi ya watu, lakini imeonekana kushindwa kupatiwa dawa, licha ya hatua kadhaa kudaiwa kuchukuliwa ikiwamo baadhi yao  kuwekwa chini ya uangalizi.

Related

Siasa 5666921514661339687

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item