jaridahuru

Mitandao

BUNGENI: KURA ZAILITABISHA BUNGE LA KATIBA, SITTA ACHANGANYA MADAWA





BUNGE Maalum la Katiba, limepitisha azimio la kuzifanyia marekebisho kanuni za 30, 36 na 38 ili kuruhusu wajumbe watakaokuwa nje ya Bunge (ndani au nje ya nchi), wapige kura za kuamua ibara na sura za rasimu ya katiba popote watakapokuwa.

Kwa mabadiliko hayo, wajumbe wa dini ya kiislamu waliokwenda hija mjini Macca nchini Saudi Arabia, wanaopata matibabu nchini India na walio katika majukumu mengine ndani na nje ya nchi, watapiga kura kuamua rasimu ya katiba mpya inayopendekezwa.

Hata hivyo, marekebisho hayo yalizua mvutano baina ya Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta na wajumbe watatu, Ezekiel Oluoch, Said Arfi na Ali Omari Juma waliopinga, ambako aliwakemea mara kwa mara wakati wakichangia, akiwaita waongo.

Kabla ya Sitta kumwita Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni, Ameir Pandu Kificho awasilishe azimio hilo, alisema kuwa wakati huu wa kukaribia kupiga kura wamelazimika kuzitazama kanuni ili kuona kama zinawawezesha kupiga kura ndani ya muda.

“Tunatarajia wapiga kura sisi wajumbe si chini ya 480, kwa jinsi kanuni zilivyokaa hivi sasa, kwamba kwa kura za wazi mjumbe anaitwa jina, halafu anatamka ndiyo au hapana kwa ibara moja baada ya nyingine na wale wa kura za siri wanakuja mbele kuandika maamuzi yao.

“Tukichukua kwamba kwa wastani kuchukua dakika mbili kwa kila mjumbe basi hizo ni dakika 960 kwa ibara moja, tunatarajia ibara zitakuwa 300, dakika 960 takribani saa 16, tukiendelea na utaratibu tutakuwa tunatumia siku nzima kwa sura moja,” alisema Sitta na kumpa nafasi Kificho.

Akiwasilisha azimio hilo kwa niaba ya Kificho, mjumbe wa kamati hiyo, Amon Mpanju, alisema kuwa kanuni ya 30 inafanyiwa marekebisho katika vifungu vya (1), (2) na kuongeza fasili mpya ya 2A.

Sasa kifungu (1) kitasomeka kuwa; akidi kwa kila kikao cha Bunge Maalum itakuwa ni nusu ya wajumbe wote wa Bunge maalum.

Fasili mpya ya “(2A) kwa madhumuni ya fasili (1) na kwa ajili ya kuzipigia kura ibara za sura za rasimu ya katiba zilizoandikwa upya na rasimu ya mwisho ya katiba, wajumbe wa Bunge maalum walio nje ya maeneo ya Bunge kwa ruhusa ya maandishi ya mwenyekiti, watajumuishwa kwenye idadi ya wajumbe waliohudhuria kwenye kikao cha Bunge.

“Kuongeza fasili mpya ya (3A) Katibu atawapatia wajumbe wa Bunge maalum waliomo ndani ya ukumbi wa Bunge orodha ya wajumbe wote waliopata ruhusa ya kupiga kura wakiwa nje ya maeneo ya Bunge maalum.

“Baada ya kanuni ya 38 kuongeza kanuni mpya ya 38A.- (1) Mjumbe yeyote aliye nje ya maneno ya Bunge maalum, anaweza kupiga kura mbele ya ofisa aliyethibitishwa kwa maandishi na Katibu wa Bunge kuwa msimamizi wa upigaji wa kura kwa masharti yafuatayo,” alisema na kuyataja;

(a) Awe ameruhusiwa kwa maandishi kuwepo nje ya ukumbi wa Bunge na mwenyekiti na (b) awe ameomba kwa mwenyekiti na kuruhusiwa kwa maandishi kupiga kura yake akiwa nje ya ukumbi wa Bunge maalum.

Baada ya kuwasilisha marekebisho hayo, Oluoch ndiye alikuwa mzungumzaji wa kwanza akisema haungi mkono wajumbe wasiokuwepo kuruhusiwa kupiga kura.

Mjumbe huyo ambaye alianza kwa kumtaka Sitta kutumia busara na kanuni kuzingatia sheria zilizopo, akisema kuwa haoni sababu ya wajumbe wasiokuwepo kulazimishwa kupiga kura kwa sababu ni kuvunja sheria.

“Kila raia wa nchi hii anayo haki ya kupiga kura akitimiza miaka 18 kikatiba, lakini haki hiyo imewekewa utaratibu kisheria, taratibu tulizo nazo hazijaweka utaribu wa kwamba mtu ambaye hatakuwepo kwenye eneo la kupigia kura ataruhusiwa kupiga kura…hatujawa na sheria hiyo,” alisema na kukatizwa na Sitta;

Kura zipi wewe unasema…Oluoch akajibu, kura yoyote ile… Sitta akauliza tena, wapi ebu nioneshe kifungu…Oluoch akaomba amalize aoneshe kifungu lakini Sitta akasema; “Unasema uongo mtupu wewe, unasema sheria ya uchaguzi, tunamchagua nani hapa?” alihoji Sitta huku Oluoch akisema “ngoja niendelee japokuwa umeniita mwongo”.

Aliongeza kuwa anachokiona ni kutaka kutimiza mambo ambayo si msingi wa sheria kwa kutaka wajumbe waliokwenda Macca kuhiji ili waweze kupiga kura, suala alilosema linahitaji ufafanuzi wa kidini kutoka kwa Sheikh Mkuu ili aeleze kama wajumbe waliokwenda kuhiji wanaweza kupiga kura.

Sitta aliendelea kuwabana wajumbe waliokuwa wakipinga azimio hilo huku akionesha kuwapendelea wale waliounga mkono kiasi cha hata wakati mwingine kuwapigia makofi walipokuwa wakichangia kwa kuingiza masuala yaliyo nje ya azimio.

Mbunge wa Mpanda Mjini (CHADEMA), naye alikumbana na kizingiti cha Sitta, pale alipokataa kuunga mkono azimio hilo akisema wenye haki ya kupiga kura ni wale watakaokuwepo siku husika.
Wakati Arfi akifafanua kwamba si haki wala busara kwa wajumbe wasiokuwepo kulazimishwa kupiga kura, akisema ni kinyume na matakwa ya demokrasia, Sitta aliingilia kati na kuhoji…nani amekwambia wanalazimishwa…nani analazimisha?

“Arfi alimjibu Sitta kwamba; “anavyotuingilia wakati tukichangia, watanzania wanakuona…unashusha hesima yako,” alisema na kujibiwa na Sitta kuwa anawajibu wa kuzungumza jambo la kweli, kwamba anaposema watu wanalazimishwa onesha ushahidi.

Hata wakati Ali Omar Jumba akichangia na kukosoa azimio hilo na kutaka shughuli ya upigaji kura isogezwe ikibidi ili waliokwenda hija wawe wamerudi, Sitta alimparamia na kumkatiza akisema; “kuna dhana inajitokeza kwamba walio nje wanalazimishwa kupiga kura. Hii sio sahihi kwani yuko mjumbe anatibiwa India ameniomba kupigia kura akiwa huko.

“Wale wanaosimama hapa na kutaka kusema kwamba tunalazimisha wajumbe, wasitupotezee muda hapa,” alisema Sitta ambaye alionekana kugadhabika.

Kwa mujibu wa Sitta, kamati ya uandishi iliomba siku moja zaidi ili kukamilisha kazi yake na kwamba rasimu ya mwisho inayopendekezwa itakabidhiwa Septemba 24 mwaka huu.

Septemba 25 wajumbe watakaa kwenye kamati kuona kama mapendekezo yao yamewekwa ipasavyo kwenye rasimu hiyo na baada ya hapo Septemba 27 na 28, kamati ya uandishi itaiweka sawa rasimu hiyo ili Septemba 29 hadi Oktoba 2 mwaka huu, ipigiwe kura.

Pia, Sitta alionekana kuwashawishi wajumbe hao, akiwataka kuipigia kura ya ndiyo rasimu inayopendekezwa na Bunge ili wamalize kazi ya kutunga Katiba na kuikabidhi kwa Rais Jakaya Kikwete ndani ya siku saba baada ya Bunge kumaliza muda wake Oktoba 4.

Related

Habari Kuu 4523195232052668271

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item