jaridahuru

Mitandao

SOKA: YANGA MTASUBIRI SANA KUVUNJA REKODI HIZI SA WEKUNDU WA MSIMBAZI - SIMBA

SIMBA na Yanga ni watani wa jadi. Jambo linalofanyika Simba kwa namna moja ama nyingine litakuwa na tambo kwa Yanga.
Simba ikishinda mchezo lazima itatoa tambo zake kwa Yanga na vivyo hivyo kwa upande wa pili. Hayo ndiyo maisha waliyoyachagua.
Yanga ndiyo bingwa wa kihistoria wa Ligi Kuu Bara ikiwa imetwaa taji hilo kwa mara 24 na kuzipiku timu nyingine zote zinazoshiriki ligi hiyo. Simba inafuatia katika rekodi hiyo baada ya kulitwaa taji hilo kwa mara 18.
Licha ya rekodi hiyo, Yanga bado inafunikwa na Simba kwenye rekodi nyingine za maana. Simba imefanikiwa kuweka rekodi kadhaa ambazo Yanga itasota kuzifikia. Makala hii inazungumzia baadhi ya rekodi za Simba ambazo Yanga inasota kuzifikia na kuzivunja.
Kucheza fainali Caf
Simba ndiyo timu pekee ya Tanzania iliyofanikiwa kucheza fainali za Kombe la Shirikisho la Vyama vya Soka Afrika (Caf), ilikuwa mwaka 1993 wakati huo likijulikana kama Kombe la Caf. Simba ilicheza fainali hiyo na Stella Abidjan ya Ivory Coast na kutoka sare katika mchezo wa awali kabla ya kukubali kipigo cha mabao 2- 0 katika marudiano jijini Dar es Salaam.
Licha ya Simba kupoteza mchezo huo ambapo wachezaji wake waliahidiwa zawadi za magari kama wangeshinda, inasalia kuwa timu pekee kutoka Tanzania Bara iliyofanikiwa kucheza hatua hiyo ya fainali hizo. Yanga imewahi kufika hatua ya makundi ya michuano hiyo.
Nusu fainali klabu Bingwa Afrika
Simba inajiweza, hivyo ndivyo unavyoweza kusema kwa lugha rahisi baada ya timu hiyo kufanikiwa kucheza nusu fainali ya Klabu Bingwa Afrika mwaka 1974. Simba iliondolewa katika hatua hiyo ya nusu fainali na Mehala El Kubra ya Misri na kuzima ndoto za kucheza fainali ya michuano hiyo mikubwa zaidi Afrika.
Rekodi hiyo ya Simba bado haijavunjwa mpaka hii leo. Yanga kwa upande wake, ilifanikiwa kucheza robo fainali ya michuano hiyo kwa mara mbili mfululizo mwaka 1969 na 1970 lakini haikuwahi kufika zaidi ya hapo.
Mbali na rekodi hiyo, Simba bado inajivunia rekodi ya kuwa timu ya kwanza kutoka Bara kufanikiwa kuiondosha timu ya Misri katika michuano ya Afrika. Simba ilifanya hivyo mwaka 2003 baada ya kuifunga Zamalek ya Misri ambayo ilikuwa bingwa mtetezi.
Ubingwa Kombe la Kagame
Licha ya Yanga kujivunia rekodi ya kutwaa taji la Kagame nje ya Dar es Salaam, Simba ndiyo vinara wa kulitwaa taji hilo nchini. Simba imewahi kulitwaa taji hilo la Kagame mara sita na kuwa timu ya Bara yenye historia ya kulitwaa zaidi kombe hilo.
Mbali na kuwa timu ya Bara iliyotwaa taji hilo mara nyingi, Simba ndiyo timu inayoongoza kwa kutwaa Kombe la Kagame kwenye historia ya michuano hiyo na kuzipiku timu zote za ukanda huo.
Yanga imewahi kulitwaa taji hilo mara tano na kuwa timu ya pili kulitwaa kombe hilo mara nyingi baada ya Simba hivyo inatakiwa kulitwaa mara moja ili kuifikia rekodi hiyo ama mara mbili ili kuivunja rekodi hiyo kabisa.
Ubingwa wa Mapinduzi
Simba imetwaa Kombe la Mapinduzi mapema wiki iliyopita huko visiwani Zanzibar na kuweka rekodi ya kulitwaa taji hilo mara nyingi zaidi kwenye historia ya michuano hiyo. Simba imetwaa taji hilo mara tatu wakati watani wao Yanga wamewahi kulitwaa mara moja pekee tangu kuanzishwa kwake miaka tisa iliyopita.
Azam ni timu ya pili kwenye rekodi hiyo ikiwa imelitwaa mara mbili. Mbali na rekodi hiyo pia Simba inaongoza kucheza mechi za fainali ya michuano hiyo ikiwa imecheza mara tano wakati watani wao wamecheza mara tatu pekee.
Kuzalisha, kuuza wachezaji
Simba ina wachezaji ambao inaweza kujivunia kuwa ni wao. Licha ya kwamba klabu hiyo inafanya usajili wa nyota kadhaa wa ndani na nje ya nchi, bado timu hiyo ina wachezaji inaojivunia kuzalishwa klabuni hapo.
Simba ina wachezaji kama Ramadhan Singano, Jonas Mkude, Said Ndemla, Abdallah Seseme na William Lucian ‘Gallas’ iliyowaibua na kuwazalisha kuwa miongoni mwa nyota wa soka nchini.
Ni wachezaji waliozalishwa klabuni hapo na kuendelezwa mpaka sasa. Wapo wengine kama Edward Christopher ‘Edo’ ambao wanacheza timu nyingine lakini chimbuko lao ni Simba. Yanga hakuna kitu kama hicho.
Kikosi cha Yanga kimejaa nyota wa kununuliwa kutoka timu nyingine za ndani na nje ya nchi. Achana na Nonda Shaaban ‘Papii’, hakuna mchezaji mwingine aliyefanikiwa kung’ara au kuuzwa nje ya nchi akitokea Yanga.
Ni rekodi ya kipekee kwa Simba ambayo itaichukua Yanga miaka mingi kuifikia. Mbali na hilo pia Simba inabaki kuwa miongoni mwa timu chache nchini zilizofanikiwa kufanya mauzo ya maana ya wachezaji nje ya nchi.
Simba ndiyo iliyomuuza Mbwana Samatta kwenda TP Mazembe. Timu hiyo ilimuuza pia mshambuliaji wa timu hiyo, Emmanuel Okwi kwenda Etoile Du Sahel ya Tunisia. Yanga haina utamaduni huo wa kuuza nyota wake.
Kipigo cha mabao 6-0
Yanga haitaki kabisa kuukumbuka mwaka 1977. Ni mwaka mchungu kwao. Timu hiyo ilifungwa na Simba mabao 6-0 kwenye mechi ya ligi shukrani kwa kazi nzuri ya Abdallah ‘King’ Kibadeni aliyefunga mabao matatu ‘hat trick’, Jumanne Hassan ‘Masimenti’ aliyefunga mawili na Suleiman Sanga aliyejifunga bao moja na kupeleka kilio hicho Jangwani. Kipigo hicho kilifuta rekodi ya Yanga ya mwaka 1968 ilipoifunga Simba mabao 5-0. Ikiwa ni miaka 37 imepita bado Yanga imeshindwa kufuta rekodi hiyo. Hali ilikuwa mbaya zaidi baada ya kufungwa tena mabao 5-0 mwaka 2012.
Msimu bila kupoteza
Simba ilifanikiwa kuweka rekodi ya kipekee mwaka 2010 baada ya kutwaa ubingwa wa ligi bila kupoteza mchezo. Ulikuwa msimu wa kipekee kwa Simba baada ya kucheza mechi 22 za msimu huo huku ikishinda 18 na sare nne. Ilikuwa ni rekodi ya kipekee.
Azam iliweza kuivunja rekodi hiyo msimu uliopita baada ya kumaliza msimu bila kupoteza mechi na kutwaa ubingwa wa Bara. Yanga haijaweza kuwa na rekodi kama hiyo na inavyoonekana itachukua miaka mingi kuivunja rekodi hiyo ya Simba.

Related

Sports 2722179143123385674

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item