jaridahuru

Mitandao

KATIBA: UKAWA WATOA MPYA, WAKWEPA JITIHADA ZOTE ZA USULUHISHI WASEMA HAWARUDI BUNGENI KUJADILI KATIBA YA CCM

MCHAKATO wa katiba mpya umefikia hatua ngumu zaidi kuliko ilivyotarajiwa baada ya wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) kutangaza rasmi kutoshiriki vikao vya maridhiano na mikutano ya Bunge Maalum.

Kwa takribani miezi miwili sasa kulikuwa na jitihada za kuwashawishi wajumbe hao kurejea bungeni baada ya kususia vikao kwa madai ya kuchoshwa na lugha za ubaguzi, matusi, kejeli na kusiginwa kwa rasimu iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Msimamo huo wa UKAWA sasa unaonyesha dhahiri huenda mchakato wa katiba ukakwama licha ya Mwenyekiti wa Bunge Maalum, Samuel Sitta kutangaza litaanza vikao vyake keshokutwa.
Kukwama kwa mchakato huo kunatokana na ukweli kuwa ili vifungu vya rasimu vipitishwe ndani ya Bunge, vitahitaji theluthi mbili ya wajumbe wote kutoka Tanzania Bara na idadi hiyo hiyo kutoka Zanzibar.

Inasadikika kuwa bila ya ushiriki wa wajumbe wa CUF kutoka Zanzibar waliomo kwenye UKAWA, theluthi mbili haitopatikana wakati wa kupiga kura.

Kutokana na jambo hilo, zipo taarifa baadhi ya vigogo wa CCM na serikali wanadaiwa kushiriki kwenye vitendo vya kuwarubuni, ikiwemo kuwapa fedha wajumbe wa CUF walio UKAWA wakiuke msimamo wa kundi lao na waingie bungeni.

UKAWA wanena
Wakizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, viongozi na wajumbe wa UKAWA, walisema hawataendelea kushiriki mazungumzo na CCM wala kuhudhuria vikao vya Bunge Maalum.

Wajumbe hao walisema kuwa hatua hiyo imefikiwa baada ya kutafakari na kuona kuwa tiba ya kuzaa katiba haijapatikana baada ya mazungumzo ya maridhiano ya kikao cha nne kilichoitishwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam kwa niaba ya wenyeviti wenza wa UKAWA, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe, alisema mazungumzo yaliyoratibiwa na Jaji Mutungi hayana faida kutokana na CCM kuendelea kudai matakwa yao na si muafaka.

Mbowe alisema ushiriki wao katika mazungumzo ya maridhiano walitarajia mabadiliko ya uendeshaji wa Bunge Maalum kwani rasimu inabeba taswira ya nini Watanzania wanataka katika katiba.

Alisema UKAWA ilitaka kuona Bunge Maalum linatekeleza wajibu wake kisheria katika kujadili, kuboresha na kupitisha rasimu ya katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kutokana na maoni ya wananchi walio wengi na si kuibomoa, kuibatilisha na kuifuta.

Alisema kuwa sura ya 83 inatambua rasmi rasimu ambayo inabeba maoni ya Watanzania, taasisi na utafiti wa kina ambazo sura zote zinaeleza serikali tatu.

Alieleza kuwa UKAWA inataka misingi iliyowekwa iheshimiwe na sio kubomoa kama ambavyo kanuni zilizowekwa na CCM zinavyoruhusu kuibomoa rasimu hiyo ili wapate kile wanachokihitaji.
Alisema kuwa CCM inatumia jeuri waliyonayo kutokana na kuwa na wabunge wengi walioongezwa kwa hila kupitia baadhi ya wajumbe 201.

Akizungumzia hotuba ya Rais Jakaya Kikwete, Mbowe alisema kuwa udhaifu aliouonyesha katika hotuba ya ufunguzi wa Bunge Maalum la Katiba ameurudia tena Julai 31, 2014 siku moja kabla ya kikao cha nne cha mazungumzo ya UKAWA na CCM.

Alisema kuwa pamoja na kauli za kuvuruga Bunge, Kikwete ndie ameukwamisha mchakato huo.
“Kikwete ameendelea kupotosha matumizi ya kanuni ya 33 ibara ya nane (i) ya kanuni za Bunge Maalum kuhusu mamlaka ya Bunge hilo na kukwepa kuzungumzia marekebisho yaliyofanyika Aprili 25, 2014 baada ya wajumbe wa UKAWA kutoka, ambapo mabadiliko hayo mapya yameingiza kanuni mpya ya 32(6) inayoruhusu Bunge Maalum kupendekeza sura mpya,” alisema.

Alisema kuwa marekebisho hayo yalilenga kupenyeza sura za rasimu ya CCM ya serikali mbili na sura nyingine zilizo kinyume na maoni ya wananchi juu ya Katiba ya Shirikisho la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mbowe, alisema msimamo potofu wa Kikwete ndio umekuwa msimamo wa wajumbe wa CCM na kukwamisha maridhiano ambayo yangewezesha muafaka wa kunusuru mchakato huo.

Alisema kuwa kutokana na kutorejea katika Bunge la Katiba, wameamua kuanza mazungumzo miongoni mwa viongozi na wajumbe wa UKAWA na wataeleza uamuzi mbadala utakaofanyika ili kuwezesha kupatikana kwa katiba ya wananchi.

NCCR-Mageuzi
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema kuwa katiba ni suala la kisiasa na si kisheria na ndiyo maana wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba hawakuchaguliwa na wananchi na kuongeza kuwa njia ya kupatikana katiba ipo ikiwa utashi wa kisiasa katika vyama hasa CCM utatolewa.

CUF
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema kuwa Rais Kikwete alipotosha hoja zao wakati UKAWA wanachohitaji ni mambo ya msingi yanayotokana na wananchi yaheshimiwe.
“Madaraka yasipore maoni ya wananchi ambayo ni mengi ndani ya rasimu ya katiba, moyo wa rasimu uko katika sura ya sita, Rais Kikwete anasema kuwa hotuba yake haikuvuruga bali alitoa maoni yake, kwanini alipoandikiwa barua na Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwa ajili ya kutoa maoni yake hakwenda, na hakutoa?

“Kwahiyo aliona sehemu sahihi ya kutoa maoni yake ni kwenye Bunge la Katiba, huo ni usanii wa mtani wangu Mkwere,” alisema.

Mnyika 
Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano wa CHADEMA, John Mnyika, alisema kuwa ili katiba ipatikane ni lazima mchakato uwe huru.

Alisema kuwa watawala wa Tanzania ndio wanaweka mazingira ya mchakato wa katiba kuleta vurugu kutokana na kuwa hakuna nia njema ya watawala wa ndani kupata katiba na kuongeza kuwa kuitegemea CCM ni kuharibu mchakato huo.

LISSU
Tundu Lissu, alisema kuwa nia ya UKAWA ni kuona yaliyomo katika rasimu ya katiba hayapinduliwi wala kubatilishwa.

“Aprili 16, 2014 UKAWA ndiyo walitoka bungeni, lakini Aprili 25, 2014 hoja ikapelekwa bungeni ya kubadili kanuni na kuweka vifungu vilivyoweza kupindua rasimu yote.

“Walijipa mamlaka ya kupindua rasimu, kanuni 32(6) ili kuingiza rasimu itakayopitisha serikali mbili, hatutarudi na hatuna ajenda nyingine zaidi ya kutaka tujadili rasimu ya wananchi,” alisema.
Lissu alisema kuwa muundo wa serikali mbili ni kasha tupu kwani Rais Jakaya Kikwete sio rais wa Zanzibar kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar.

“Muundo wa serikali tatu utatuokoa na hautasambaratisha nchi, haiwezekani nchi moja iwe na Amiri Jeshi Mkuu wawili, serikali tatu ndio njia pekee ya kuwa wamoja,” alisema.

Hoja za UKAWA kugoma kurudi kabisa katika Bunge Maalum la Katiba ni kutotaka kusaliti maoni ya wananchi na kutumia vibaya fedha za umma kubariki uchakachuaji wa msingi wa rasimu.
Pia kutaka kanuni zilizobadilishwa wakati UKAWA hawapo zifutwe na lugha za uchochezi, ubaguzi, udini, dharau, dhihaka na matusi ndani ya Bunge hilo zikomeshwe na badala yake mamlaka ijikite katika kuboresha rasimu na misingi yake kwa kuzingatia maoni ya wananchi.

Kakobe amlaumu Kikwete
Askofu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF), Zachary Kakobe, amemshambulia Rais Kikwete kwamba ndiye aliyevuruga mchakato wa kupatikana kwa katiba mpya.
Kakobe amewataka wajumbe wa UKAWA kutorejea katika Bunge Maalum la Katiba ambalo alidai limejazwa unafiki na endapo wakiamua kurejea watakuwa wamerogwa.

Alitoa kauli hiyo jana jijini Dar es Salaam katika maadhimisho ya miaka 25 ya kanisa hilo lililoanzishwa mwaka 1989.

Alisema Rais Kikwete, alipolizindua Bunge Maalum la Katiba, alitumia fursa hiyo kutoa hoja za kuvuruga rasimu ya wananchi ambayo iliwasilishwa na Jaji Joseph Warioba.

Askofu Kakobe alisema hoja za Rais Kikwete za kujikanganya alizozitoa siku hiyo, yalikuwa ni majibu ya maombi ya Jumuiya ya Wakristo wa Kipentekoste (PCT) ya kuvuruga mchakato wa katiba baada ya kutoa upendeleo kwa kuwateua baadhi ya wajumbe wakiwamo viongozi wa dini, kupata uwakilishi kwa baadhi ya Wakristo bila kutenda haki kwa wananchi wote.

Alisema katika mambo yanayofanywa makusudi na wanadamu, Mungu amewapa akili ya kuyavuruga, hivyo ndiyo maana wakiwa katika viwanja vya Sabasaba waliamua kufanya maombi na nguvu ya Mungu inatumika sasa kuonyesha kuwa mchakato huu ulianzishwa pasipo haki.

“Namtaka Rais Kikwete akiri hadharani kuwa amekosea na awaombe Watanzania radhi kwa makosa aliyoyafanya hata kusababisha wanasiasa upande wa upinzani kuunda UKAWA ili haki ya wananchi ipatikane, hivyo atumie busara kufanya hivyo kwa kuwa ndiye baba wa taifa hili.

“Kuna kauli za viongozi wa CCM kuwa wanataka kutawala milele… sasa mimi nasema sawa tu wafanye hivyo, lakini kwa kwenda na haki na siyo kwa kulazimisha kama ilivyo sasa katika suala la katiba… hivyo ni katiba ya wananchi wote wa Tanzania ambao wamo vyama vya siasa na wasiokuwemo,” alisema.

Askofu Kabobe alisema katika kujikweza kuwa hajahusika kuvuruga, Rais Kikwete, amewatumia vibaya viongozi wa dini aliodai wanaegemea upande wa CCM kuwataka waombee mchakato wa katiba na kuwataka UKAWA warudi bungeni, huku akijua watumishi hao wanapaswa kufanya kazi isiyo na upendeleo.

“Daima nitasimama katika kweli nayo itaniweka huru, hapa nasema wazi kwamba Rais Kikwete ameamua kuwatumia vibaya viongozi wa dini… nao wakaona bora watumike ili kupata mkate na chai Ikulu ambayo majani yake ni ya hapahapa nchini, tena Mufindi, siyo dhahabu, wanachoendelea kukifanya kwa wanachi ni unafiki wala siyo maombi.

“Nilidhani Rais Kikwete atawaambia viongozi hao wamwombee yeye aliyevuruga mchakato huu na siyo kuuombea mchakato wa katiba na amani… mimi najua nchi yetu ina amani na amani itavurugwa na hao wanaong’ang’ania hoja zao, kwani katika hili gumzo la katiba linaloendelea mtu mjinga tu ndiye atakayewalaumu UKAWA.

“Nawaomba viongozi wa dini wasijikombe kombe Ikulu maana wao wanamwakilisha Mungu… siogopi kusema kwa sasa hakuna ninachokosa hapa duniani wala sitaki kupendwa na rais, nitafanya yampendezayo Mungu,” alisema.

Huku akirudia rudia neno lake kwamba “sema ukweli ili uwe huru”, Askofu Kakobe alisema anawaunga mkono UKAWA kwa hatua yao waliyofikia hadi sasa hadi hapo Rais Kikwete atakapoomba radhi na kukubali wakajadili rasimu ya wananchi, kama watarudi bila makubaliano hayo, basi watakuwa wamerogwa.

“Nawaunga mkono UKAWA asilimia 100 kwa 100 na ninawaongeza 50 kwa hatua yao… sasa warudi kwa kauli ya rais kukiri mbele ya wananchi kuwa amekosea, anajirekebisha ili wajadili rasimu ya katiba, wasipofanya hivyo basi watakuwa wamerogwa… hakuna maridhiano hapo maana nimefuatilia na kubaini mazungumzo yanayoendelea yamejawa unafiki.

“Kuwaunga mkono UKAWA kwangu si kwamba nashabikia chama kimojawapo kinachounda umoja huo hapana… nazungumza kama baba wa kiroho mwenye kuwachunga watoto wengi wenye vyama vyote vya siasa ambavyo vipo nchini, ambao wanajua kwamba ninasimamia ukweli tupu,” alisema.

Mdahalo wa wanasheria
Watanzania wametakiwa kuwa makini ili kuzuia kutoingia katika machafuko kama yale yaliyotokea nchini Kenya baada ya kukosekana kwa katiba.

Akitoa mtazamo wake jana jijini Dar es Salaam katika mdahalo uliokuwa na mvutano wa makundi yaliyokuwa yakikinzana katika suala la mchakato wa katiba mpya, Profesa Patrick Lumumba, amewasihi Watanzania kutopita njia ambazo ni hatari kufikia upatikanaji wa katiba mpya.

“Msipite njia ambayo wengi hawakupita katika kutafuta amani, kwanini mvuke maziwa na mzame kwenye madimbwi, tuwashurutishe wanasiasa wasitupitishe njia iliyopitwa na wengi kwa kumwaga damu,” alisema.

Prof Lumumba alisema kuwa wazalendo wengi nchini wanahitaji katiba mpya na bado wana imani kuwapo nafasi ya kuipata bila kupigana.

Kwa upande wa UKAWA kugoma kurudi bungeni, Prof. Lumumba alisema kuwa wana sababu za kususia Bunge Maalum la Katiba kwani msingi wake ni kujadili rasimu.
Alisema kuwa ujumbe wa UKAWA umeshafika ingawa inaonyesha rais ameshakubali kwamba aliteleza na hawezi kukiri.

Alisema kuwa Watanzania asilimia 99 wanataka rasimu ya katiba ijadiliwe na sio katiba ya wanasiasa.

“Watanzania wanataka watu waache itikadi zao, wasimamie Utanzania wao, Watanzania wanasema, ikiwa hatuwezi kupata katiba kabla ya uchaguzi, basi tufanye mabadiliko yanayotakiwa na kisha tuwape jukumu serikali itakayochaguliwa kusimamia upatikanaji wa katiba mpya inayotakiwa na Watanzania,” alisema.

Prof. Lumumba alieleza kuwa yeye kama Mkenya anafuatilia kuhusu Tanzania na kueleza kuwa siasa za nchi hii si za kikabila, lakini zina matatizo.

Alieleza kuwa wananchi ndio wenye katiba na sio ya wanasiasa waliokwatua madaraka hayo.
“Bunge kazi yake ni kuboresha na sio kubadili na hiyo inafanyika duniani kote, ikitokea nyie mkabadili mtakuwa wa kwanza duniani, na wananchi wanatakiwa wahakikishe waliyoyatoa kwenye tume yamo, je wakikuta hakuna itakuwaje?” alihoji.

Kwa upande wake, Jenerali Ulimwengu alisema kuwa udhaifu wa viongozi unaweza kuwa ulichangia kukwama na kufika hapo katiba ilipo.

“Baadhi walidhani katiba ndiyo mwanzo wa kukidhoofisha chama tawala na waliopinga nao pia walidhani wanaweza ondolewa madarakani,” alisema.
Alieleza kuwa watawala walianza kuchafua mchakato toka kutungwa kwa sheria ya mabadiliko ya katiba ya awali iliyoanza.

Related

Siasa 3713680948522396519

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item