jaridahuru

Mitandao

BIASHARA: PINDA ATAKA MAONESHO YA SABASABA YASIMAMISHWE



Dar es Salaam. Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameshauri Maonyesho ya Kimataifa ya Biashara ya Mwalimu Julius Nyerere, maarufu kama Sabasaba, yasimamishwe angalau kwa mwaka mmoja kwa ajili ya kurekebisha miundombinu ndani ya uwanja huo ili iendane na viwango vinavyostahili.

Pinda alisema hayo jana alipotembelea maonyesho hayo ya kila mwaka yanayoendelea kwenye uwanja huo kukagua mabanda mbalimbali ya kampuni zinazotangaza biashara na taasisi binafsi na serikali zinazotoa huduma mbalimbali.

“Nimemshauri Waziri wa Viwanda na Biashara kuwa viwanja hivi vinahitaji marekebisho. Ongezeko la washiriki wa kimataifa ambao nimeambiwa zimefikia kampuni 500 kutoka nchi 33, inadhihirisha umuhimu na kukua kwa maonyesho yenyewe ambayo sasa nchi mbalimbali zinayazingatia,” alisema Pinda.

“Ikibidi tupoteze fursa ya mwaka mmoja ili tuboreshe viwanja hivi tulivyorithi na kuendelea kuvitumia kwa muda mrefu vikiwa na miundombinu ileile. Yatupasa kuboresha kila kitu kwa viwango vya kimataifa. Ukihudhuria maonyesho mengine ya kimataifa katika nchi nyingine unaona tofauti ya ubora wa viwanja vyao ukilinganisha na hivi vyetu… njia ni ndogo na hazijapangwa vizuri.”

Mbali na barabara za ndani ya uwanja huo kuwa ndogo, mpangilio mbovu wa mabanda ya maonyesho, umeme kukatika mara kwa mara, uchache wa maliwato na kutokuwapo kwa alama za kuongoza magari yanapoingia hadi kutoka, vimekuwa ni vitu vinavyolalamikiwa sana na washiriki wa maonyesho hayo makubwa kwenye ukanda wa mashariki ya Afrika.

Waziri Mkuu alitembelea mabanda kadhaa na kujionea shughuli zinazofanywa ambapo alivutiwa na ubora unaoonekana katika bidhaa nyingi za kilimo na kupendekeza umakini kidogo uongezwe katika ufungaji wa bidhaa hizo.

“Mnajua kuwa napenda sana asali. Kuna maendeleo makubwa sana nimeyaona kutoka kwa wakulima waliopo kwenye banda la asali… wamejitahidi kuongeza ubora na wanatia moyo kwa kuwa kila mmoja anaweza akaliona hilo miongoni mwa bidhaa zilizopo,” alisema Waziri Mkuu na kueleza kuwa changamoto aliyoiona katika vifungashio akiiomba mamlaka husika kuwaongezea uwezo wafugaji wa nyuki.

Pinda aliitaka sekta binafsi kuisaidia Serikali kuboresha huduma za kijamii hasa elimu ya juu baada ya juhudi za Kampuni ya Global Education Link kumfahamisha wanavyoshughulika katika kupeleka wanafunzi nje kufuata taratibu na sheria zilizopo ili wakanufaike na kuja kulitumikia taifa baadaye.
“Juhudi za vijana kama hawa zinapaswa kupongezwa na kuungwa mkono. Wazazi wengi wamekuwa wakipoteza fadha kusomesha watoto wao nje na pale warejeapo wanakataliwa na bodi ya vyuo vikuu lakini kwa namna hawa jamaa wanavyofanya kazi yao kwa uwazi na gharama nafuu. Nashauri vijana wengi zaidi wajitokeze ili kupunguza urasimu uliopo serikalini,” alisema Pinda.

“Hakuna taasisi ya serikali inayoweza kukuambia kuwa wanatoa ufadhili kama hawa vijana. Sisi serikali zikiwepo nafasi hizo ni mpaka mtu atafute taarifa, tena kwa shida ndipo azipate.”
Kwa jumla, Pinda alipongeza juhudi za Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara (TanTrade) kwa kuboresha na kuyatangaza maonyesho hayo kimataifa kiasi cha kushawishi kampuni nyingi kutoka nchi tofauti kuja kushiriki.

“Maonyesho kama haya yana nafasi nzuri ya kuimarisha uchumi wa nchi kama kampuni ya ndani yatatumia ipasavyo fursa waipatayo kujenga uhusiano mzuri na wenzao wa nje kwa kuwa itawasaidia kujua mahitaji yaliyopo katika nchi mbalimbali waliko na washirika,” alisema.

Related

Events 2267561996414400421

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item