Dodoma. Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa
amesema vijana 10,500 waliojitokeza hivi karibuni kwenye Uwanja wa
Taifa, Dar es Salaam kufanya usaili wa nafasi 70 za kazi katika Idara ya
Uhamiaji, ni ishara kuwa bomu la ajira litalipuka muda wowote.
Akizungumza na waandishi wa habari jana nje ya
Viwanja vya Bunge, Lowassa alisema Serikali ni lazima ihakikishe
inatengeneza ajira kwa kuwa kila mwaka zaidi ya vijana 30,000 wanahitimu
katika vyuo mbalimbali nchini.
Wasomi hao wa fani mbalimbali walijitokeza katika
uwanja huo Ijumaa iliyopita, kuanzia saa 12 asubuhi wakisubiri kufanyiwa
usaili huo.
Lowassa ambaye alijiuzulu wadhifa wa Waziri Mkuu
mwaka 2008, amenukuliwa mara nyingi akiitaka Serikali kuchukua hatua
kukabiliana na tatizo la ajira na akisema ni bomu linalosubiri kulipuka.
Mbunge huyo wa Monduli kupitia CCM, aliwahi
kuingia kwenye malumbano makali na Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia
Kabaka kuhusiana na suala la ajira kwa vijana.
Kabaka akiwa bungeni, Machi 21, 2012 alitoa
takwimu za namna Serikali ilivyokuwa inatengeneza ajira kwa nia ya
kumjibu Lowassa, ambaye alikuwa ameeleza tatizo la ajira linavyowaathiri
vijana.
Jana, Lowassa kuongezeka kwa makundi ya vijana
wanaopora watu katika maeneo mbalimbali nchini ni ishara ya ukosefu wa
ajira. “Watanzania sasa tupo milioni 48 na kila mwaka vijana zaidi ya
30,000 wanahitimu vyuo vikuu na kazi hakuna, pamoja na hilo hatuambiwi
ni vijana wangapi ambao hawana kazi,” alisema Lowassa.
Alisema lazima Serikali itengeneze ajira kwa
wananchi wake, huku akimtolea mfano Rais wa Marekani, Barack Obama
kwamba alishinda awamu ya pili kwa sababu ya kutengeneza ajira.
“Mfano mzuri ni katika uanzishwaji wa viwanda.
Tunapofikiria kuanzisha kiwanda cha pamba kwanza lazima tuangalie
tutatengeneza ajira ngapi,” alisema.
Katika kuonyesha kuwa ajira sasa ni tatizo nchini,
juzi jioni wakati wa mjadala wa Bajeti Kuu, Naibu Spika Job Ndugai
alisema Mtanzania mwenye nia ya kugombea urais mwaka 2015 ili aweze
kuelekewa kwa wananchi ni lazima aeleze mikakati ya kuwasaidia vijana
kupata ajira.
“Ajira ni tatizo kubwa na lazima lishughulikiwe.
Kuna vijana hawaendi shule lazima watazamwe. Kuna wanaomaliza darasa la
saba, kidato cha nne, cha sita na vyuo vikuu. Nazungumza kutoka moyoni
kabisa. Hizi ni dakika za mwisho za Serikali ya awamu ya nne, wale
wanaojipanga kwa awamu ya tano kama hawataongelea ajira basi waandike
wameumia.”
Ndugai alisema vijana wasio na kazi ndiyo
wapigakura wakubwa na kusisitiza kuwa mgombea yeyote makini ni lazima
afikirie suala la ajira kwa vijana.
Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe alisema:
“Vijana 10,500 kufanya usaili wa nafasi 70 ni janga la taifa. Yupo
kiongozi mmoja mwandamizi wa CCM aliwahi kulizungumza hili lakini
akapondwa kwamba anazungumza mambo kwa kuzua. Sasa huu ndiyo ukweli
wenyewe.”