jaridahuru

Mitandao

BUNGENI: BAJETI KUU YA SERIKALI 2014/2015 HATIMAYE YAPITISHWA

 

Dodoma. Bajeti Kuu ya Serikali ya 2014/15 imepitishwa jana bungeni mjini hapa na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya akisema lazima wafanyabiashara walipe kodi inayostahili na iwapo kuna anayedhani anapata hasara kwa kulipa kodi afunge biashara.
Akihitimisha mjadala wa bajeti hiyo kabla ya umeme kukatika wakati wa upigaji kura kuipitisha, Mkuya alisema kama mfanyakazi anatozwa kodi, mfanyabiashara anayepata faida hataachwa.
“Mfano hata hapa Dodoma wanakuja kuzungumza na ninyi wabunge ili kuanza kuwafanyia ushawishi ili muwasaidie katika kukwepa kodi, hilo haliwezekani,” alisema.
Alikemea wizi wa fedha za umma unaofanywa na watumishi wa Serikali akisema unaumiza taifa na kuifanya Serikali ipate hasara kubwa.
“Mfano kuna wakati mtu mmoja alileta taarifa za kuidai Serikali Sh600 milioni, lakini tulipokwenda kuhakiki tukagundua kuwa alikuwa anadai Sh600,000 tu, sasa wabunge tunaposema kuna wizi, basi lazima muamini kuwa huo ndiyo wizi wa mali ya umma,” alisema Mkuya.
Alisema uhakiki huo ulipunguza deni la taifa kutoka Sh19 bilioni hadi Sh5 bilioni ambalo ndilo deni halisi kwa wadai wa ndani.
Mkuya alisema kuanzia sasa, Serikali haitalipa fedha zozote za deni hadi uhakiki ufanyike kwa kuwa wizi umezidi ikiwamo katika ununuzi wa magari na sasa hakutakuwa na taasisi itakayoruhusiwa kununua magari yake hadi kwa kibali maalumu cha Hazina na yote yatanunuliwa kwa pamoja kutoka kwa mzalishaji bila kupitia mawakala.
“Katika hilo tumejipanga pia kuhakikisha kuwa hatupeleki fedha katika taasisi zozote ambazo hazitaleta ripoti ya utekelezaji.”
Kuhusu suala la mikopo, alisema kuwa Tanzania itaendelea kukopa kwa ajili ya maendeleo kwa kuwa deni la taifa linahimilika kwa vyanzo vyake vyote, hivyo kusema wasikope siyo sahihi.
Akizungumzia suala la magari chakavu ambalo lilipigiwa kelele na wabunge wengi, alisema msimamo wa Serikali utabaki hivyo kwamba magari yanayoanzia umri wa miaka minane na kuzidi ni lazima yatozwe ushuru mkubwa.
Alisema wamefanya hivyo baada ya kubaini kuwa Tanzania imefanywa kuwa dampo la kutupa magari mabovu kutoka maeneo mbalimbali duniani.
Alisema baada ya kubaini kuwa magari yaliyozidi muda huo yamepandishwa kodi hapa nchini, bei za magari ya Toyota nchini Japan zimeshuka.

Awali, Kamati ya Bajeti ililieleza Bunge kwamba Serikali imeridhia kuongeza Sh115 bilioni kwa ajili ya kujazia fedha zilizopungua kwa wizara mbalimbali.
Akizungumzia misamaha ya kodi, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba alisema lengo la kufuta kwa misamaha ya kodi isiyo na tija ni kuiongezea Serikali mapato na siyo kufukuza wawekezaji nchini.
Akiwasilisha mapendekezo ya Kamati ya Bajeti, Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dk Festus Limbu alisema Sh8.2 bilioni ziliongezwa katika Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ajili ya maboresho ya Jeshi la Polisi ili kuimarisha mafunzo na vitendea kazi.
“Sh14.4 bilioni zimeongezwa kugharimia mahitaji ya ziada ya kuhamisha makato ya kodi ya mishahara Zanzibar kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Sh16 bilioni zimeongezwa katika Wizara ya Mambo ya Nje kwa ajili ya kugharimia mahitaji mapya ya Balozi za Comoro, The Hague pamoja na safari za viongozi,” alisema Dk Limbu.
Alisema Sh13.7 bilioni zimeongezwa katika Wizara za Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Kitengo cha Ngome kwa ajili ya kulipa posho na Sh12.45 bilioni zimeongezwa katika Mfuko wa Bunge kwa ajili ya kugharimia Bunge la Katiba.
“Sh5. 8 bilioni zimeongezwa Tamisemi kwa ajili ya kugharimia matengenezo ya barabara, Sh1.25 bilioni zimeongezwa katika Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo kwa ajili ya kulipia deni la Televisheni ya Taifa (TBC), Bunge na maadhimisho ya sherehe za Muungano. Wizara ya Ujenzi imeongezewa Sh43.36 bilioni kugharimia matengenezo ya barabara,” alisema.

Related

Habari Mpya 6051979134627918921

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item