jaridahuru

Mitandao

ELIMU: MFAHAMU PIUS MSEKWA, MTANZANIA MWENYE ELIMU NA UJUZI USIOTIA MASHAKA



Wakati Tanzania inapata uhuru wake mwaka 1961, haikuwa na wasomi wengi ila wa kuhesabu, hasa wa ngazi ya chuo kikuu.
Mmoja wao, ni spika mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Pius Chipanda Msekwa.

Kama ilivyokuwa kwa wasomi wenzake wengi wakiwa wamepitia Chuo Kikuu cha Makerere, hakuwa kando katika uongozi wa nchi.

Akiwa mwanafunzi mtiifu wa Mwalimu Julius Nyerere tangu wakiwa Pugu, alijikuta akikabidhiwa majukumu ya kuwa mmoja wa watendaji muhimu wa serikali ya Tanganyika huru na  chama cha TANU.

Ukiondoa kazi ya Ukatibu wa Bunge aliyoanza mwaka 1960 akiwa na miaka 25, mwaka 1967 akiwa na umri wa miaka 32 aliteuliwa kuwa Katibu Mtendaji Mkuu wa TANU.
Kwa umri na elimu yake huo ulikuwa muda wa kuifaidi dunia, achilia mbali kufanya kazi za kuutumikia umma.
Kwa vijana wa sasa,  hicho ndicho kipindi cha kupupia maisha badala ya utumishi uliotukuka kwa umma.

Miaka zaidi 50  ya utumishi wa umma na kama mwanasiasa,  Msekwa ambaye ni msomi mwenye weledi mkubwa katika historia, sayansi ya siasa, uongozi wa umma na sheria ya katiba na utawala, anasema hakufikiria kutumia madaraka yake kwa maslahi binafsi, seuze kutapanya mali ya umma.
Mfano mzuri wa urithi ambao vijana wa sasa hawana budi kujifunza kwake ni namna alivyokubali nyumba yake binafsi iliyopo kisiwani Ukerewe kutumiwa na viongozi wa juu nchini bila kudai chochote kwa serikali.

“ Ni nyumba nzuri...wakubwa wote wakienda wanafikia kwangu, maDC ma RC wote wanajua hivyo, wanalala bure tu ni wageni wangu, sitaki kujilimbikizia mali, ‘’ anaeleza.

Msekwa anajua kulipa fadhila kwa jamii hasa akikumbuka kuwa mafanikio yake kielimu yalitokana na msaada wa wasamaria wema waliomsaidia baada ya baba yake kufariki dunia.

Tarikhi yake inaonyesha baada ya baba yake kufariki akiwa darasa la tano, alipata udhamini na mfanyabiashara mmoja mwenye asili ya bara la Asia mpaka alipomaliza shahada ya kwanza katika Chuo Kikuu cha Makerere.

“Niliguswa sana na wema huo, niliendelea kukumbuka na kuenzi kitendo chake hicho wakati wote…. Kwa ajili hiyo baadaye sana katika maisha yangu nilipokuwa nimepata uwezo wa kufanya hivyo, nilihamasika kuwatendea watu wengine wema kama huo, anasema katika kitabu chake kiitwacho ‘Uongozi na Utawala wa Mwalimu Julius Nyerere’.

Anaongeza kusema kuwa fadhila zaidi kwa jamii alitoa alipokuwa Spika wa Bunge alipoamua kujenga shule ya sekondari  katika kijiji alichozaliwa, Bugombe kisiwani Ukerewe na baadaye kuikabidhi kwa serikali.  Shule hiyo inajulikana kwa jina la Pius Msekwa Secondary School.

Maisha ya shule
Tangu akiwa ngazi za chini za elimu hadi chuo kikuu, alidhihirisha uwezo mkubwa wa kuyakabili masomo ikiwamo lugha ya Kiingereza aliyoimudu barabara.

Kwa mfano, alipokuwa sekondari alipewa tuzo ya tabia njema na bidii katika masomo. Darasa la 12 alifaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza mtihani uliojulikana kwa jina la Cambridge School Certificate na hivyo kupata fursa ya kuchaguliwa kusoma katika Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda.

Akiwa chuoni hapo aliendelea kudhihirisha ‘ukali’ wake katika masomo kwa kushinda zawadi ya fedha baada ya kuibuka mshindi katika uandishi wa insha katika somo la Uchumi.
Aidha, alipokuwa Makerere ndipo alipoanza kupata uzoefu wa uongozi kwa kuchaguliwa kuwa katibu mkuu chama cha wanafunzi wa chuo hicho.
Akiongoza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

Kuanzia mwaka 1970 hadi 1977 alikuwa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, fursa anayosema ilimwezesha kwa kiasi kikubwa kumtumia Mwalimu Nyerere kwa ushauri wa namna bora ya kuendesha chuo hicho.

Anasema alikiongoza chuo hicho katika kipindi ambacho wanafunzi walikuwa wachache na waliochaguliwa kwa malengo maalumu ya utumishi wa umma. Ndiyo maana kila aliyemaliza alikuwa na uhakika wa ajira.

Msekwa ameacha historia ya aina yake chuoni hapo kwani wakati akiiongoza taasisi hiyo iliyosheheni wasomi mahiri, hakusita kuomba nafasi ya kusomea shahada ya uzamili. Aliamua kuwa mwanafunzi wa wale aliokuwa akiwaongoza.

Kwa mujibu wa kitabu chake hicho, uamuzi wa kusoma katika chuo alichokuwa akikiongoza anasema ulitokana na ushauri wa Mwalimu Nyerere aliyemwambia: ‘’ Wewe kiongozi wa wasomi na walio wengi zaidi miongoni mwao ni wanafunzi. Kwa hiyo ukiamua kuwa mwanafunzi utafanana nao.’’

Mwandishi wa vitabu
Msekwa ni mmoja wa viongozi wachache nchini wenye mapenzi na sanaa ya uandishi, Ameandika vitabu zaidi ya saba baadhi vikiwa vinatumika kama rejea katika taasisi za elimu ya juu.

Baadhi ya vitabu hivyo ni Essays on The Transition to Multi-partism in Tanzania (1995), 50 Years of Independence: A concise Political History of Tanzania (2013), Reflections on Tanzania’s multi-party Parliament (2000) na Uongozi na utawala wa Mwalimu Julius Nyerere: Miaka 25 ya utumishi wa umma chini ya uongozi wa Mwalimu Julius Nyerere.

Vingine ni Towards Party Supremacy (1977), Education Policy Formation Before and After the Arusha Declaration (1979), Parliament Privilege in Tanzania (2003) na Insha za ufafanuzi wa baadhi ya masuala ya chama (1982).

Wasifu wake
Kwa mujibu wa maelezo yaliyomo katika kitabu chake, ‘Uongozi na Utawala wa Mwalimu Julius Nyerere: Miaka 25 ya utumishi wa umma chini ya uongozi wa Mwalimu Julius Nyerere, Pius Msekwa alizaliwa katika kijiji cha Bugombe wilayani Ukerewe mwaka 1935.
Elimu ya msingi alisoma katika Shule ya Msingi Kagunguli wilayani humo na baadaye elimu ya  sekondari katika shule za  Nyegezi, Mwanza na kilichokuwa Chuo cha Mtakatifu Francis (sasa sekondari ya Pugu).

Alichaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu kishiriki cha Makerere alipohitimu Shahada ya Kwanza katika somo la Historia,  Machi 1960.

Hadi anaamua kupumzika, Msekwa alifanya kazi katika nafasi mbalimbali kama Katibu wa Bunge, Katibu Mtendaji Mkuu wa TANU, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Katibu Mtendaji wa Chama cha Mapinduzi, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Makamu Mwenyekiti wa CCM.

Related

Elimu 3740472910042286569

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item