jaridahuru

Mitandao

SIASA: MAMBO MATANO YALIYOIBUKA KATIKA ZIARA YA KINANA TABORA


Katibu mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana amekuwa akifanya ziara katika mikoa mbalimbali nchini.

Kwa siku 11 alikuwa Tabora na kutembelea Igunga, Nzega, Uyui, Sikonge, Urambo, Kaliua na Tabora Mjini.

Kinana akiwa na katibu wake wa itikadi na uenezi, Nape Nauye walikagua uhai wa chama na kukutana na changamoto nyingi katika ziara hiyo ambazo wananchi wa Tabora wanataka zipatiwe ufumbuzi.

Ujenzi wa bomba la maji
Wilayani Igunga na Nzega lilijitokeza tatizo kubwa la maji na wananchi wakakumbuka ahadi iliyowahi kutolewa na Rais Jakaya Kikwete ya ujenzi wa bomba la maji kutoka Ziwa Victoria hadi mkoani humo.

Hivi sasa bomba hilo kutoka Ziwa Victoria linaishia mkoani Shinyanga.
Mwenyekiti wa CCM wa Tabora, Hassan Wakasuvi alimweleza Kinana kuwa tatizo la maji ni kubwa na kwamba wananchi wa mkoa huo wanaikumbuka ahadi iliyotolewa na Rais kwamba angewaletea maji kutoka Ziwa Victoria.

“Mkoa huu ni ngome ya CCM kwa sababu wabunge wote na zaidi ya asilimia 90 ya madiwani ni wa CCM. Tunaomba katibu mkuu ukamkumbushe Rais kwamba tunaomba ahadi yake itekelezwe kabla hajamaliza kipindi chake cha uongozi mwaka 2015,” alisema.

Baada ya kuwasiliana na Serikali, Kinana alisema kwamba serikali wakati wowote kuanzia sasa itasaini mikataba ya upembuzi yakinifu na michoro ikiwa ni maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa bomba la maji kutoka Shinyanga kwenda Tabora.

“Tena nimeongea na Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe kwamba mikataba hiyo isainiwe Tabora ili wananchi waweze kushuhudia kuanza kwa mradi huo,” anasema na kuongeza kwamba wakati upembuzi huo ukifanyika Serikali inatafuta fedha za ujenzi wa bomba hilo.

Hifadhi ya Misitu
Kilio kikubwa kilichotolewa na wanachama wa CCM ni ufinyu wa ardhi kwa ajili ya makazi na kilimo na ufugaji.

Kilio hicho kiliungwa mkono na mkuu wa mkoa, Fatma Mwasa ambaye alisema asilimia 70 ya ardhi ya mkoa huo ni hifadhi ya misitu na asilimia 30 ndiyo inayotumika kwa ajili ya kilimo.

Hali ni mbaya zaidi kwenye Wilaya ya Sikonge ambayo asilimia 95 ya ardhi `imefunikwa’ na misitu ambayo ni hifadhi ya misitu ambayo hairuhusiwi kuitumia kwa shughuli za kibinadamu.

Wana-CCM ambao ni wafugaji walilalamikia kukamatwa na maofisa misitu kila wakati mifugo inapoingia kwenye hifadhi na kuomba Serikali iongeze eneo la matumizi ya binadamu kwa sababu watu wanazidi kuongezeka. Akijibu hilo, Mwassa anasema ameshapeleka mapendekezo Wizara ya Maliasili na Utalii ili waweze kushughulikia tatizo hili.

“Katibu mkuu hili ni tatizo kubwa katika mkoa huu. Tunaomba maeneo ya hifadhi yamegwe kwa sababu idadi ya watu hivi sasa inazidi kuongezeka. Hakutakuwa na maana kutenga eneo la hifadhi kubwa wakati wananchi wanapata shida,” anasema. Kinana kwa upande wake aliahidi kufuatilia suala hilo serikalini.

Zahanati
Mkuu wa Wilaya ya Igunga, Elibariki Kingu alitoa kilio cha wananchi kwamba licha ya kuhamasisha wanavijiji kujitolea kujenga zahanati katika kijiji na kufanikiwa kujenga zahanati 70, tatizo ni kwamba hazijasajiliwa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii hivyo hazijaanza kufanya kazi kwa sababu hakuna nyumba za watumishi.

“Wanavijiji wanatembea umbali mrefu kutafuta huduma za afya huku majengo yao ya zahanati yakiwa yamekamilika, tunapoulizwa na wananchi kwa nini hazijafunguliwa tunapata wakati mgumu kuwajibu, tunaomba wizara iache urasimu,” alisema.

Majibu ya Kinana
Kinana anasema huo ni urasimu wa viongozi wa wizara hiyo na kwamba atafuatilia ili zahanati hizo ziweze kusajiliwa.

“Sababu inayotolewa kwamba ni lazima zahanati ziwe na nyumba za wauguzi ndipo zifunguliwe hazina maana. Mbona walimu wanapelekwa kwenye shule ambazo hazina nyumba? Hatuwezi kuwaacha wananchi wateseke wakati zahanati zipo,” alisema Kinana.

Tumbaku
Tumbaku ni zao kubwa la biashara ambalo linategemewa na wakazi wa mkoa huo, lakini katika miaka ya hivi karibu limekuwa halina tija kwa sababu ya ufisadi wa baadhi ya viongozi wa vyama vya ushirika mkoani humo.

Katika kipindi cha miaka miwili, wakazi wa mkoa huo wanadai Sh28 bilioni kwa vyama vya ushirika vilivyopo kwenye mkoa huo.

Mbunge wa Sikonge, Said Nkumba anadai kuwakataza wananchi kuuza tumbaku kwenye vyama hivyo kwa sababu ya ufisadi wa viongozi kwa kuwa wanawakopa huku wakiwa hawana uhakika kama watawalipa fedha hizo.

Nkumba anasema mwaka juzi, Wizara ya Kilimo, Ushirika na Chakula ilifanya uchunguzi kuhusu tumbaku na kubaini ufisadi mkubwa, lakini hakuna hatua zilizochukuliwa licha ya ripoti hiyo kutolewa. Waziri wa wizara hiyo, Christopher Hiza hajachukua hatua zozote kuwawajibisha waliohusika na ufisadi huo.

Mkuu wa mkoa, Mwasa naye alipigilia msumari kwamba Injinia Chiza ameshindwa kuwachukulia hatua mafisadi wa tumbaku, hali ambayo inasababisha asieleweke kwa jamii.

Alisema wamefikia hatua ya kuwaruhusu wananchi kuuza tumbaku yao popote penye soko ambalo litawapatia fedha bila kukopwa. “Haiwezekani kuwa na watu wanaoishi Dar es Salaam ambao wananufaika na tumbaku kwa ufisadi wakati wakulima wakiendelea kuwa maskini kwa miaka mingi,” anasema.

Akizungumzia hilo, Kinana alisema matatizo ya wakulima wa tumbaku ni ya muda mrefu na akaahidi kwamba tatizo hilo linatakiwa kumalizika. “Nitakwenda kuzungumza na rais ili tatizo hilo liweze kufikia kikomo, hatuwezi kuendelea na tatizo hili tena ni lazima achukue hatua zitakazomaliza tatizo hili.”

Majengo yatelekezwa
Majengo saba ambayo yalitakiwa kujengwa vituo vya afya chini ya mpango wa kunusuru vifo vya kinamama yametekekezwa bila kumalizika katika zabuni iliyotolewa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa mkandarasi, Humphrey Contractors wenye thamani ya Sh2 bilioni. Nkumba alimweleza Kinana kwamba majengo hayo yapo wilayani Sikonge lakini yameshindwa kukamilika. Anasema mkataba wa ujenzi huo ulikuwa ukamilike tangu mwaka 2002 lakini hadi sasa yamebaki `mapagale’.

“Tunashindwa kufahamu nini kimetokea, wizara imekaa kimya, mkandarasi haendelei na ujenzi, tumebaki tunashangaa,” alisema. Kinana alishangazwa na kitendo cha wizara hiyo kuingia mkataba na mkandarasi huyo badala ya kazi hiyo kufanya na Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ambayo ingekuwa rahisi kufuatilia.

“Nashangaa watu wanavikubali vyeo wakati hawana uwezo wa kuwatumikia wananchi, wanakaa ofisini wakati mambo huku yanaharibika, kwa nini hawavikatai vyeo hivyo, hawa ndiyo aina ya viongozi wanaofanya sherehe wakati wakiteuliwa huku wakiwa hawana uwezo wa kufanya kazi,” alisema.

Kinana alisema atapambana hadi aone nini kilitokea kwenye zabuni hiyo na kwamba atawajulisha wakazi wa Sikonge atakapobaini ukweli.

“Nitapambana nao hadi kieleweke, kazi ya chama ni kusimamia Serikali kutekelezaji ya ilani ya chama, kama kuna ufisadi katika zabuni hii mtajulishwa na hatua zitachukuliwa,” alisema.

‘Nukuu’
Viongozi tuwe wasikivu kwenye matatizo ya watu

Related

Siasa 2122955447621964797

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item