jaridahuru

Mitandao

MEI MOSI : Je unajua maana ya Mei Mosi?



NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI UINGEREZA
Wewe hufikiria nini unaposikia Mei Mosi? Magwaride na maandamano? Kucheza dansi kuzunguka nguzo ya Mei? Au, siku ya mapumziko?
IKITEGEMEA unakoishi, watu huwa na maoni tofauti-tofauti kuhusu Mei Mosi. Hata hivyo, maoni hayo yanatokana na chanzo kimoja. Kuchunguza kifupi chanzo cha Mei Mosi kutatusaidia kuelewa maana ya siku hiyo leo.

Asili ya Mei Mosi
Katika Roma ya kale, siku ya kwanza ya Mei ilikuwa sikukuu ya Floralia, iliyopewa jina la Flora, mungu wa majira ya masika na wa maua. Ulikuwa wakati wa kuimba, kucheza dansi, na magwaride yaliyopambwa kwa maua. Makahaba wa Roma hasa waliifurahia sikukuu hiyo, kwa kuwa walimwona Flora kuwa mungu wao mkuu.

Waroma walipoanza kumiliki nchi nyingine, walisambaza desturi zao huko. Hata hivyo, katika nchi za Kiselti, Waroma walitambua kwamba tayari siku ya kwanza ya Mei ilikuwa ikiadhimishwa ikiwa sikukuu ya Beltane. Jioni iliyotangulia sikukuu hiyo, mwanzo wa siku ya Kiselti, mioto yote ilizimwa, na jua lilipochomoza, watu waliwasha mioto mikubwa kwenye vilele vya vilima au chini ya miti mitakatifu ili kukaribisha majira ya kiangazi na mwanzo mpya wa uhai. Ng’ombe walipelekwa malishoni, nayo miungu iliombwa ilinde ng’ombe hao. Muda si muda, Floralia na Beltane ziliungana na kuwa sikukuu ya Mei Mosi.
Huko Ujerumani na katika nchi za Skandinavia, sikukuu hiyo iliitwa Walpurga. Sherehe zilianza Usiku wa Walpurga kwa kuwasha mioto mikubwa ili kufukuza wachawi na pepo. Katika nchi nyingine za Ulaya, Mei Mosi iliadhimishwa kwa njia tofauti-tofauti, na baadhi ya njia hizo zingalipo.
Makanisa ya Kikristo hayakuwa na uvutano mkubwa katika sikukuu hizo za kipagani. Gazeti moja la Uingereza (Guardian) linasema: “Katika kalenda, Mei Mosi—au Beltane—ndiyo iliyokuwa siku ambayo kila mtu angefanya apendavyo, sikukuu pekee ambayo kanisa la Kikristo au mamlaka nyingine yoyote haingeweza kudhibiti.”

Desturi za Mei Mosi
Kufikia Enzi za Kati, desturi mpya zilikuwa zimeongezwa katika sikukuu hiyo iliyopendwa sana huko Uingereza. Wanaume kwa wanawake walikesha vichakani wakikusanya maua na matumba ili ‘kuukaribisha mwezi wa Mei’ jua likichomoza.* Kulingana na trakti moja ya Philip Stubbes (The Anatomy of Abuses), uasherati ulikuwa umeenea sana. Wapenda-anasa walisimamisha Nguzo ya Mei katikati ya kijiji, ambapo watu walicheza dansi na michezo mingine wakiizunguka nguzo hiyo mchana kutwa. Stubbes aliiita nguzo hiyo “Sanamu yenye kuchukiza.” Watu walimteua malkia wa Mei, na mara nyingi pia walimteua mfalme wa Mei, ili kusimamia sherehe hizo. Katika sehemu mbalimbali za Ulaya pia, kulikuwa na Nguzo za Mei na malkia wa Mei.
Desturi zote hizo za Mei Mosi zilikuwa na umuhimu gani? Kichapo kimoja (Encyclopædia Britannica) kinaeleza hivi: “Mwanzoni sherehe hizo zilikusudiwa kuhakikisha kwamba kungekuwa na mazao mengi, na pia ng’ombe na watu wangezaana kwa wingi, lakini katika visa vingi kusudi hilo la awali lilipotea pole kwa pole, na mazoea hayo yakaendelezwa katika sherehe zinazopendwa na wengi.”

Mapendezi Mbalimbali
Wanaharakati wa Uprotestanti walijaribu kuondolea mbali sikukuu hiyo iliyoonwa kuwa ya kipagani. Scotland iliyokuwa imeathiriwa na mafundisho ya Calvin ilipiga marufuku sikukuu ya Mei Mosi katika mwaka wa 1555. Kisha Bunge la Uingereza lililokuwa likiongozwa na Waprotestanti likapiga marufuku Nguzo za Mei katika mwaka wa 1644. Katika kile kipindi cha Jumuiya ya Madola, wakati ambapo hakukuwa na mfalme huko Uingereza, “mazoea mapotovu” ya Mei Mosi yalipigwa marufuku. Hata hivyo, katika mwaka wa 1660, kulipokuwa na mfalme tena, Nguzo za Mei zilianza kutumiwa tena.
Sherehe za Nguzo ya Mei zilipungua hatua kwa hatua katika karne ya 18 na mwanzoni mwa karne ya 19 lakini zimeanza kuongezeka tena hivi karibuni pasipo upotovu uliokuwapo awali. Desturi nyingi za Mei Mosi, kama vile watoto kucheza dansi wakizunguka Nguzo ya Mei wakisokota tepe zenye rangi mbalimbali, zimeanza majuzi. Hata hivyo, watafiti wa desturi za awali za Mei Mosi wanagundua mambo mengi ya kipagani yanayohusiana na chanzo cha sikukuu hiyo.
Watu waliohama Ulaya walipeleka desturi za Mei Mosi walikoenda, na baadhi ya wazao wao bado husherehekea sikukuu ya Mei Mosi kidesturi. Hata hivyo, katika nchi nyingi Mei Mosi, au Jumatatu ya kwanza baada ya tarehe moja Mei, ni sikukuu ya wafanyakazi.

Mei Mosi Yawa Sikukuu ya Wafanyakazi
Magwaride na maandamano ya sikukuu ya kisasa ya Mei Mosi yalianzia Amerika Kaskazini. Kwa nini? Yale mapinduzi ya viwanda yalitokeza mashine zilizofanya kazi mfululizo, na kwa hiyo wenye viwanda waliwataka wafanyakazi wafanye kazi mfululizo kwa saa 16 hivi kila siku isipokuwa Jumapili. Ili kuboresha maisha ya wafanyakazi, vyama vya wafanyabiashara na wafanyakazi huko Marekani na Kanada vilitaka kuanzia Mei 1, 1886 siku ya kazi iwe na urefu wa saa nane. Waajiri wengi walikataa ombi hilo, kwa hiyo maelfu ya wafanyakazi waligoma Mei tarehe 1.
Kwa mara ya kwanza kabisa wanaharakati wa wafanyakazi waliuawa katika Ghasia za Haymarket huko Chicago, Illinois, Marekani, na wafanyakazi wengine nchini Hispania, Italia, Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, na Urusi, waliunga mkono harakati hizo.* Mnamo mwaka wa 1889, mkutano wa vyama vya Kisoshalisti ulimwenguni huko Paris ulitangaza kwamba Mei 1, 1890, ingekuwa siku ya kimataifa ya maandamano ya kutetea siku ya kazi ya saa nane. Kuanzia wakati huo, Mei 1 ikawa sikukuu ya kila mwaka ya kutetea masilahi ya wafanyakazi.
Katika jamhuri za Muungano wa Sovieti, kwa kawaida Mei Mosi ilisherehekewa kwa magwaride ya kijeshi na maonyesho ya maendeleo ya kiteknolojia. Nchi nyingi leo husherehekea Siku ya Wafanyakazi tarehe moja Mei. Hata hivyo, Marekani na Kanada husherehekea siku hiyo Jumatatu ya kwanza ya Septemba.

Uhusiano Kati ya Sikukuu ya Kale na ya Leo
Sikuzote Mei Mosi imekuwa sikukuu ya umma. Wafanyakazi hawakwenda kazini iwe waajiri wao walikubali au la. Majukumu yalibadilika. Watu wa kawaida walimwigiza mfalme na malkia, na mara nyingi watawala walidhihakiwa kwa utani. Kwa hiyo, Mei Mosi ilikuja kuhusianishwa na harakati za wafanyakazi, na kufikia karne ya 20, ilitambuliwa na chama cha Kisoshalisti kuwa sikukuu.
Kama sikukuu ya kale ya Mei Mosi, Siku ya Wafanyakazi Duniani imekuwa siku ya magwaride mitaani. Hata hivyo, katika miaka ya karibuni kumekuwa na jeuri katika sherehe za Mei Mosi. Kwa mfano, mnamo Mei Mosi mwaka wa 2000, kulikuwa na maandamano ulimwenguni pote ya kupinga ubepari. Waandamanaji walipigana, walijeruhiwa na kuharibu mali.

Kuleta Mabadiliko Yanayohitajiwa
Je, kweli tunaweza kutazamia wanadamu walete mabadiliko yanayohitajiwa ulimwenguni pote kwa faida ya watu wote wanyoofu? Hawawezi. Methali moja ya kale ya Biblia imethibitika kuwa kweli: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Nguvu zinazozidi za wanadamu zinahitajiwa ili kuleta amani ulimwenguni. Chanzo cha nguvu hizo ni Yehova Mungu, Muumba wa dunia. Neno lake Biblia, linasema kwamba ‘anaufumbua mkono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’ (Zaburi 145:16) Tunakutia moyo uchunguze zaidi ahadi za ajabu za Mungu.
Ili kutimiza sala ya kielelezo ambayo Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, aliwafundisha wafuasi wake, Ufalme wa Mungu utakuja na bila shaka mapenzi ya Mungu yatatendeka duniani. Biblia inaahidi kwamba Yesu Kristo, Mtawala aliyewekwa rasmi na Mungu, “atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.”—Zaburi 72:12-14.

[Maelezo ya Chini]
Kabla ya kalenda ya Gregory kuanza kutumiwa miaka 400 hivi iliyopita, mwezi wa Mei ulianza siku 11 baadaye kinyume na ilivyo leo, wakati ambapo kulikuwa na joto na mimea mingi zaidi.
Ghasia hizo zilizuka siku moja baada ya wafanyakazi kadhaa kufa katika mapambano kati ya waandamanaji na polisi wa kutuliza ghasia.

[Picha katika ukurasa wa 12]
Nguzo ya karne ya 16 ya sikukuu ya Mei iliyosimamishwa kila Mei Mosi nje ya kanisa huko London

[Hisani]
From the book Observations on Popular Antiquities

[Picha katika ukurasa wa 14]
Maandamano ya kupinga ubepari, Mei Mosi mwaka wa 2000, London, Uingereza

[Hisani]

© Philip Wolmuth/Panos Pictures

Related

Kitaifa 4017253467458064877

Post a Comment

emo-but-icon

Wadhamini

UJUMBE

JH Katika Facebook

Nyayo zetu twitter

Za Juu

Mitandao

Piga Kura

Je ungependa Tanzania iwe na serikali ngapi?
  
pollcode.com free polls 

ADVERTISEMENTS

Msimamo wa ligi mbalimbali

Football results provided by whatsthescore.com

Mechi Live

Walioko Hewani Kwa Sasa

item